KWA ufupi ni kama Yanga imesema: “Kama noma na iwe”, hiyo ni baada ya
kutoa kauli kuwa imekata rufaa ya kufungiwa kwa mchezaji wao, Mrisho
Ngassa, kucheza mechi sita na kulipa Shilingi milioni 45 ambapo imeamua
kulipeleka suala hilo kwa Mahakama ya Usuluhishi wa Michezo (Cas)
iliyopo Uswis.

Akizungumza na gazeti hili, Katibu Mkuu wa Yanga,
Lawrence Mwalusako, amesema licha ya kuwa rufaa yao ipo mikononi mwa
Shirikisho la Soka la Tanzania (TFF), lakini kuna kila dalili kuwa Simba
wamemsajili mchezaji huyo ‘kimagumashi’, hivyo adhabu za Fifa zipo wazi
kuwa viongozi wa timu hiyo wanatakiwa kufungiwa siyo chini ya miezi 12.
Alisema
wanaamini Ngassa ni mchezaji wao halali na watapeleka malalamiko yao
Cas ikiwa wataona haki haijatendeka, kwani wanaamini Ngassa amefungiwa
kwa vifungu ‘hewa’.
Mwalusako amesema adhabu iliyotolewa haijataja
vifungu vya sheria ya kumwadhibu
Ngassa, pia kama ni kweli alisaini
mkataba na Simba, kwa vile mikataba iliyopo inaonyesha alifanya hivyo
kabla ya kipindi cha miezi sita ya mkataba wake wa Azam kumalizika,
hivyo Simba nao walikiuka sheria na wanastahili kuadhibiwa.
“Sheria
za usajili zinasema mchezaji anaweza kusaini makubaliano na timu
nyingine akibakiza miezi sita kabla ya mkataba wake wa awali kufikia
tamati, lakini karatasi zilizopo zinaonyesha Ngassa alisaini mkataba huo
wa Simba kabla ya kipindi hicho kufika.
“Maana yake kama ni adhabu
hata Simba wanatakiwa kuadhibiwa, lakini kumfungia mchezaji kucheza
mechi sita ni kuiadhibu Yanga kwa kosa ambalo halihusiki.
“Kamati ya
Sheria na Hadhi za Wachezaji ya TFF ambayo imetoa adhabu hiyo haijaweka
wazi kifungu cha kanuni Yanga au Ngassa waliyokiuka. Yanga inaiona
adhabu hii kuwa ni ya uonevu kwa klabu na mchezaji, hivyo
tumeshawasilisha barua ya pingamizi tangu Agosti 23, 2013,” alisema
Mwalusako.
Mwalusako ameeleza kuwa mazingira yaliyokuwepo na
kuripotiwa kwenye vyombo vya habari likiwemo suala la usajili wa
mchezaji huyo kutoka Azam kwenda Simba na kipindi alipotaka kusajiliwa
na El Merreikh, yanaonyesha Ngassa alikuwa akilazimishwa kufanya maamuzi
mengi.
“Ngassa alikataa kwenda Simba kwa kudai kuwa hawezi kuuzwa
kama mbuzi, yaani bila kushirikishwa, baadaye alitishwa kuwa kama
asingeenda Simba basi angekaa benchi mpaka mwisho wa mkataba wake.
“Suala
la kujiuliza ni kwa nini mkataba waliosaini Simba na Azam tarehe
2/8/2012, haukuizuia Simba kupinga uuzwaji huo? Jibu ni rahisi kwamba
mkataba haukuwa na nguvu yoyote ya kikanuni au kisheria, ndiyo maana
Simba hawakupinga.
“Mwongozo wa Fifa juu ya hadhi za wachezaji na
masuala ya kinidhamu kipengele cha 3(d) unaeleza kuwa katika kuhakikisha
udhibiti wa mkataba baina ya mchezaji na klabu, mahusiano ya kiajira
lazima yazingatie uwiano wa pande zote mbili.
“Kifungu cha 3(f) cha
mwongozo huo kinabainisha kuwa kuna vipindi viwili tu vya usajili katika
msimu mmoja. Je, Simba waliingia makubaliano na Ngassa katika kipindi
kipi mbali na kuwa katika mkopo kwa msimu mmoja?
“Ngassa hakuwa na
mkataba halali na Simba, inakuwaje awajibishwe kinidhamu na Kamati ya
Sheria na Hadhi za Wachezaji kwa makubaliano ambayo hayatambuliwi
kikanuni na kisheria?
“Lakini pia Ngassa hakupewa nafasi ya kujitetea
juu ya utata wa yanayosemekana makubaliano ya kumpa fedha. Kama
ilithibitika Ngassa kapokea fedha, ni kiasi gani? Na kama alipewa gari,
thamani yake ni kiasi gani? Hivyo vyote huthibitishwa kwa risiti au
‘bank statement’,” alisema.
BONGO NEWS 4 NEWS#
No comments:
Post a Comment