Habari na Happiness Katabazi
MFANYABIASHARA Amadi Ally Popi (35), jana alifikishwa katika
Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu Dar es Salaam, akikakabiliwa na makosa
mawili likiwemo la kughushi barua inayoonyesha imeandikwa na Waziri
Mkuu, Mizengo Pinda.
Mbele ya Hakimu Mkazi Waliarwande Lema, Inspekta wa Polisi Hamis Said
alidai tarehe na siku isiyofahamika ndani ya jiji la Dar es Salaam, kwa
nia ya kudanganya Popi alighushi barua yenye kumbukumbu
Na,DA21/3078/01A/142 ya Desemba 3, 2012 akijaribu kuonyesha kuwa barua
hiyo ni halali na ilikuwa imeandikwa na kusainiwa na Waziri Mkuu,
Pinda.
Alidai shtaka lingine ni kuwa tarehe na siku isiyofahamika ndani ya
jiji la Dar es Salaam, bila ya kuwa na mamlaka yoyote alitengeneza
barua hiyo na kuisani na kisha alimpatia Islamu Mohammed Mtila
akijaribu kuonyesha barua hiyo imetoka katika Ofisi ya Waziri Mkuu na
imesainiwa na Pinda.
Mshtakiwa huyo alikana tuhuma hizo na kupelekwa rumande baada ya
kushindwa kutimiza masharti ya dhamana ya kuwa na wadhamini wawili
wanaofanya kazi serikalini au kwenye taasisi zinazofahamika watakaosaini
bondi ya sh milioni 10.
Pia mmoja wa wadhamini hao kuwasilisha mahakamani hati ya mali
isiyohamishika yenye thamani hiyo. Kesi itatajwa Septemba 5 mwaka huu
kwa kuwa upepelezi wake haujakamilika.
Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Jumamosi Agosti 24 mwaka 2013.
No comments:
Post a Comment